Saturday 8 October 2011

NI YAKO MAISHA.


NI YAKO MAISHA.                                         24th Nov, 2010

1) Maisha yako maisha, usiwe mshika dau,
Maisha yako maisha, kuwa wewe mwenye dau,
Maisha yako maisha, sije ukaisahau,                
Maisha yako maisha, jitose ndani ya dau.

2) Maisha yako maisha, maisha yako mashuwa,
Maisha yako maisha, nahodha ndiwe hasuwa,
Maisha yako maisha, jaribu piga hatuwa,
Maisha yako maisha, fanya hima kukuwa.

3) Maisha yako maisha, rafikizo wanapaa,
Maisha yako maisha, hata nawe unafaa,
Maisha yako maisha, kurudi nyuma kataa,
Maisha yako maisha, tazama mwendo wa saa.

4) Maisha yako maisha, mwendo ni mrefu kabisa,
Maisha yako maisha, mbio anza sasa,
Maisha yako maisha, usiwachwe nyuma hasa,
Maisha yako maisha, maisha ukawa tasa.

 5) Maisha yako maisha, maisha yako ni maua,
Maisha yako maisha, sijaribu kuyaua,
Maisha yako maisha, jitahidi kufufua,
Maisha yako maisha, yahitaji kuyajua.

6) Maisha yako maisha, omba na yatakupisha,
Maisha yako maisha, Mola atayahuisha,
Maisha yako maisha, jaribu kuyaendesha,
Maisha yako maisha, dereva ni wewe kisha.

7) Maisha yako maisha, tamati nimefika,
Maisha yako maisha, nasaha imenitoka,
Maisha yako maisha, dunia yetu hakika,
Maisha yako maisha, jaribu kubidiika.

No comments: